Wednesday 5 September 2012

MAREHEMU DAUD MWANGOSI AZIKWA KIJIJINI KWAO BUSOKA

Mjane wa marehemu Daud Mwangosi akilia kwa uchungu  juu ya kaburi la mumewe  mara baada ya  mazishi
 MAZISHI ya Mwandishi wa Habari, Daud Mwangosi yalifanyika jana katika Kijiji cha Busoka kilichoko wilayani Rungwe, Mbeya na kuhudhuriwa na mamia ya waombolezaji wakiongozwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Profesa Mark Mwandosya na Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa. 

Katika mazishi hayo, viongozi hao wawili kila mmoja alitangaza kuwasomesha watoto wa marehemu Mwangosi ambaye alifariki dunia Septemba 2, mwaka huu baada ya kupigwa na kitu kinachodhaniwa kuwa ni bomu wakati polisi walipokuwa wakisambaratisha mkutano wa Chadema.

Tuesday 4 September 2012

KATIBA MPYA KUPATIKANA APRIL, 2014


TUME ya Mabadiliko ya Katiba imesema imejipanga kukamilisha majukumu yake ndani ya muda uliowekwa na Sheria ya Mabadiliko ya Katiba, hivyo nchi kuwa na Katiba Mpya ifikapo Aprili, mwaka 2014.

Mwenyekiti wa tume hiyo, Jaji mstaafu Joseph Warioba, aliwaeleza mawaziri wa Katiba na Sheria kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuwa pamoja na changamoto zilizopo, dhamira hiyo ya tume ipo palepale.

Mawaziri hao, Mathias Chikawe wa Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Abubakar Khamis Bakari wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar walitembelea ofisi za Tume ya Mabadiliko ya Katiba jana, ili kujionea utekelezaji wa shughuli mbalimbali za tume hiyo.

Sunday 2 September 2012

KATIBU WA CCM MKOA WA MOROGORO AFARIKI

Katibu wa CCM mkoa wa Morogoro Bi. Asha Kipangula afariki dunia jana tarehe 1/09/2012 majira ya asubuhi katika hospitali ya TMJ Mikocheni,alipokuwa anauguzwa kutokana na maradhi yatokanayo na kujaa kwa lehemu (Cholesterol).

Mwili wa marehemu umeagwa leo asubuhi saa tatu katika hospitali ya rufaa ya Muhimbili kwa safari ya kwenda mkoani Iringa kwa mazishi.Taarifa zilizopo ni kwamba Mwili wa marehemu utapitishwa katika ofisi za chama mkoani Morogoro kwa ajili ya taratibu ya ndugu,jamaa,viongozi na wanachama wa mkoani hapo kutoa heshima zao za mwisho kwa mpendwa wao kabla ya kuendelea na safari ya kuelekea Iringa baadae mchana.


                "MUNGU AILAZE ROHO YA MAREHEMU MAHALI PEMA PEPONI" 

GEITA DOCUMENTARY

Contributors