Wednesday 15 April 2015

KWAPAMOJA TUSAIDIANE KUPAMBANA NA AJALI ZINAZOMALIZA WATANZANIA WENGI:



Kila kitu kinawezekana,, Hivi ndivyo Shule ya Jangwani ilivyoshinda tuzo ya ujasiriamali..

MAKALA YA MWANANCHI.

Wanafunzi wa shule ya wasichana ya Jangwani wakionyesha baadhi ya kazi wanazojifunza. Picha na Maimuna Kubegeya

Programu ya mafunzo ya ujasiriamali kwa wanafunzi, ni malumu kwa ajili ya kuwaandaa kuingia kwenye dunia ya biashara

        Hivi karibuni, Shule ya Sekondari ya Wasichana ya Jangwani, iliibuka mshindi kwenye shindano la ujasiriamali kwa ajili ya wanafunzi wa shule za sekondari za jijini Dar es Salaam.
Shindano hilo lilitokana na mafunzo ya miezi mitatu kuhusu ujasiriamali yaliyokuwa yakitolewa kwa wanafunzi wa shule zaidi ya 10 za jijini humo na Taasisi isiyo ya kiserikali ya Junior Achievment Tanzania (JAT).
Kufikia kilele cha mafunzo hayo, shule zilizoshiriki zilipata wasaa wa kushindana na hatimaye, Jangwani iliibuka kinara na kujishindia nafasi ya kuiwakilisha Tanzania kwenye mashindano ya kimataifa yatakayofanyika nchini Gabon Disemba mwaka huu.
Nafasi ya pili ilichukuliwa na Shule ya Benjamin Mkapa, huku Chuo cha Ufundi Stadi Kipawa kikichukua nafasi ya tatu.
Shule nyingine zilizoshiriki ni pamoja na Shule za sekondari za Pugu , Kibasila, Middland, Tegeta na Jitegemee pamoja na vyuo vya Paradgims, Chuo cha Ufundi Stadi Kipawa na Chang’ombe.
Mkurugenzi wa kampuni E-Smart Creators ya Jangwani, Sonia Apolo, anasema kuwa siri pekee ya ushindi wao ni ule ubunifu waliotumia katika kutengeneza bidhaa yao ya kipekee.
“Mkaa wa makaratasi ndio bidhaa iliyotupa ushindi na hata kuweza kupata nafasi hii. Tulitumia muda wetu mwingi kujifunza tukiwa kwenye programu hii ya mafunzo na baada ya kufuzu, tuliuingiza kwenye biashara” anasema na kuongeza:
“Mkaa huu unatumika kwa kupikia na hata kuongeza joto majumbani kwa maeneo yenye baridi, hivyo mipango yetu ya baadaye ni kuhakikisha bidhaa yetu inawafikia Watanzania wengi.”
Pamoja na bidhaa hii ya kipekee, shule ya Jangwani ilionyesha bidhaa zake nyingine walizoziingiza sokoni ikiwa ni baada ya kuuza hisa na kupata mtaji wa kuendesha biashara yao.
Miongoni mwa bidhaa hizo zilikuwa ni pamoja na fulana zilizochapishwa nembo ya kampuni yao, bangili, hereni na vifaa vya shule.
Shindano la ujasiriamali
Mratibu wa programu hiyo, Hamis Kasongo anasema kuwa shindano hilo ni miongoni mwa programu za kawaida zinazoendeshwa na taasisi yake, zikilenga kumtayarisha kijana wa Kitanzania kuingia kwenye ulimwengu wa biashara, huku akijua thamani halisi ya pesa na matumizi yake.

“Tumekuwa tukiendesha programu mbalimbali kwa vijana wa rika tofauti tofauti. Baadhi yake ni pamoja na program ya kampuni, ‘Its tyme’, Job shadow na nyingine nyingi zikiwa na nia ya kumuandaa kijana kupambana na ulimwengu wa kibiashara” anafafanua.
Anasema kuwa wanafunzi hufundishwa jinsi ya kuendesha kampuni, wakianza kujitengenezea mfumo wa kampuni na baadaye kununua hisa zinazowawezesha kuanzisha mradi utakaweza kuwaingizia pesa.
Katika mfumo huo, anasema kunakuwa na wakurugenzi na pia mameneja wanaoratibu kazi za kila siku na hatimaye kufanikiwa kutengeneza faida.
Program hiyo inayoendeshwa kwa miezi mitatu pia hutoa fursa kwa vijana hao kujifunza jinsi ya kuandika michanganuo ya kibishara na pia ripoti wakati wa kufunga hesabu za kampuni.
Meneja wa masoko wa benki ya Baclays, ambao ndio wadhamini wa program hiyo, Joel Bendera, anasema kuwa mpango wao ni kuhakikisha vijana wengi zaidi wanapata mafunzo hayo, kwani licha ya kuwapanua kiuelewa, yatasaidia kuwapa ujasiri wa kujiajiri mara wamalizapo masomo yao.
“Tangu kuanzishwa kwa programu hii mwaka 1998, tumekuwa mstari wa mbele kuhakikisha vijana wengi zaidi wanafikiwa. Tutahakikisha kila mwaka tunakuwa bega kwa bega na JAT, ili kufikia malengo yetu” anaeleza,
Ushuhuda
Issac Uswege ni mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Mzumbe,tawi la Mbeya ambaye ni miongoni mwa wanafunzi waliopitia programu hiyo.
“Nilifanya programu hii nikiwa Shule ya Sekondari Tambaza wakati ule nilitekeleza majukumu kama mkurugenzi. Nikiwa katika wadhifa wangu huo nilifanikiwa kutengeneza mikakati iliyoboresha kampuni yetu na hata kufanikiwa kupata ushindi kwenye mashindano kama haya” anafafanua
Anasema mafunzo hayo yalimjenga kiujasiriamali hata kumshawishi kufungua biashara yake binafsi mara baada ya kumaliza kidato cha sita.
“Nilianza na biashara ya pikipiki na baadaye niliziuza na kununua bajaji. Nilianza kufanya biashara wakati nasubiri matokeo yangu lakini hata baada ya kutoka matokeo na kufaulu, bado niliendelea na biashara huku nikisoma katika Chuo Kikuu cha Mzumbe” anasema na kuongeza.
“Hivi sasa nimemaliza masomo nimeajiriwa kama mwalimu wa biashara, lakini pia naendelea na ujasiriamali. Kwa sasa nimejikita katika kilimo cha miti” anafafanua. Junior Achievment ni taasisi iliyoanzishwa nchini Marekani na imeenea katika nchi 121 duniani, zikiwamo 15 zilizopo barani Afrika. Hadi sasa imetoa mafunzo kwa vijana zaidi ya vijana 25,000.

GEITA DOCUMENTARY

Contributors