Friday 30 November 2012

KUELEKEA MAADHIMISHO YA SIKU YA UKIMWI DUNIANI



KESHO Desemba mosi ni Siku ya Maadhimisho ya Ukimwi Duniani.
Hivyo basi kwa kuwa ni miaka kadhaa sasa tangu maadhimisho hayo yaanze kufanyika ni wajibu wa kila mmoja kuamua kwa dhati kuadhimisha siku hii.
Pia yatupasa kuwakumbuka ndugu jamaa na marafiki wetu ambao wamepoteza maisha kutokana na ugonjwa huu wa upungufu wa kinga mwilini.

Kila Mtanzania ana wajibu wa kuwa balozi mwema katika siku hii ambayo imesababisha watoto wengi kubaki yatima kutokana na kupoteza wazazi na walezi wao.
Sisi wa Tanzania Daima tunasema elimu tambuzi bado ni muhimu kwa kila Mtanzania kuwa mwalimu kwa mwenzake kama tunataka kutokomeza ugonjwa huu.
Ingawa kuna dawa za kupunguza makali ya virusi vinavyosababisha ukimwi (ARV,s) huku kinamama wajawazito wakiweza kutuzimia dawa za kumkinga mtoto asipatwe na maabukizi isiwe kichocheo cha watu kuendelea kuendekeza vitendo vya uasherati.
Tunasema wakati sasa umefika kwa kila mmoja wetu kwenda kupima ili kujitambua hali kama ni nzima basi kuacha mambo ya uasherati na kama tayari umeathirika fuata taratibu za kunywa dawa na kufuata ushauri unaopatiwa kliniki na matabibu wahusika.
Hata hivyo, tunasema wanafamilia wanapaswa kuketi pamoja na kupeana elimu ya namna ya kujilinda na kujikinga ili kupunguza maambukizi zaidi.
Kundi la vijana ndilo kundi linaloongoza kwa maambukizi kiasi kwamba hali hivi sasa inatisha kama siyo kuogofya jamii.
Aidha Wizara ya Afya na Ustawi wa Jamii inalo jukumu kubwa la kusaidia kutoa elimu hii kwa jamii.
Nguvu zaidi zielekezwe katika kila jambo linalofanyika ikiwa ni pamoja na mikutano ya kidini, siasa pamoja na makundi mbalimbali ya sanaa na muziki nchini na kwenye kumbi za burudani, ikibidi muziki uzimwe kwa sekunde kadhaa halafu litolewe tangazo kwamba ukimwi unaua chukua tahadhari.
Tunaamini hali hiyo itasaidia kubadili tabia ya watu na ujumbe utakuwa umefika kwa wahusika wake.

No comments:

GEITA DOCUMENTARY

Contributors