Wednesday 24 October 2012

NDEGE YA JESHI YAANGUKA, MMOJA APOTEZA MAISHA


MWANAJESHI mmoja amefariki dunia na mwingine kujeruhiwa baada ya ndege ya mafunzo waliyokuwa wamepanda maofisa wa Jeshi la Wananchi nchini (JWTZ) kupoteza mwelekeo na kuanguka katika eneo la Ukonga jijini Dar es Salaam jana.

Akizungumza na gazeti hili jana, Msemaji wa Jeshi hilo, Kanali Kapambala Mgawe, alisema kuwa ndege hiyo ilikuwa haijaruka, lakini maelezo yake yameonekana kujichanganya.

Alisema wakati ndege hiyo ikijiandaa kuruka ikiwa na maofisa wa mafunzo wawili, ilipoteza mwelekeo na kuserereka na kuelekea ndani kwenye hanga kitendo kilichowafanya waamue kujinusuru maisha yao.

“Ndani ya hanga hilo kulikuwa na ndege nyingine mbili, lakini hata hivyo tunashukuru hakuna madhara yaliyotokea, kila kitu kiko salama,” alisema Kanali Mgawe.

Alisema wanajeshi hao, kila mmoja aliamua kuchumpa kwa mwamvuli ambapo Kapteni Magushi alianguka juu ya paa la jengo lililokuwa karibu na eneo hilo ndipo alipopoteza maisha.

Alimtaja mwanajeshi aliyenusurika katika tukio hilo, kuwa ni Kapteni Kwidika, ambaye amekimbizwa katika hospitali ya kijeshi Lugalo jijini Dar es Salaam kwa ajili ya kupatiwa matibabu.
Wanajeshi hao walikuwa katika shughuli zao za mafunzo ya kawaida.

No comments:

GEITA DOCUMENTARY

Contributors