Thursday 3 May 2012

Watu saba wafa ajali ya basi la NBS

WATU saba wamekufa papo hapo na wengine 54 wamejeruhiwa baada ya basi la Kampuni ya NBS lenye namba za usajili T 978 ATM lililokuwa likitokea mkoani Tabora kuelekea mkoani Arusha kupinduka katika eneo la Jineri, nje kidogo ya mji wa Igunga.

Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tabora Anthony Lutta, alisema kuwa ajali hiyo ilitokea majira ya saa nne asubuhi katika eneo hilo baada ya kupasuka kwa matairi ya mbele, na kusababisha gari hilo kukosa mwelekeo na kugonga mti.

Baadhi ya abiria waliohojiwa na Tanzania Daima walisema kuwa chanzo cha ajali hiyo ni mwendo kasi ambao ulisababisha kupasuka kwa matairi hayo.

Mganga Mkuu wa Hospitali ya Wilaya ya Igunga Joseph Kisala alisema wamepokea miili ya watu saba, kati yao wanaume watatu na wanawake watatu na mtoto mmoja wa kiume ambapo miili yao imehifadhiwa katika chumba cha kuhifadhia maiti katika hospitali hiyo.

Aliwataja marehemu waliotambuliwa kuwa ni Anna Kisima, Dickson Nassani pamoja na Zainabu Hamdu.

Kisima aliongeza kuwa majeruhi watano wanatarajiwa kupelekwa katika Hospitali ya Rufaa Bugando, Mwanza kwa matibabu zaidi kulingana na uhaba wa vifaa vya matibabu vya Hospitali ya Wilaya ya Igunga.

Aliwataja majeruhi hao wanaotarajiwa kupelekwa Hospitali ya Rufaa Bugando kuwa ni pamoja na Iddi Hussein (34) ambaye ni dereva wa basi hilo, Kasongo Athumani (36) na wengine watatu ambao majina yao hayakuweza kupatikana.


Kwa hisani ya Tanzania Daima

No comments:

GEITA DOCUMENTARY

Contributors